Pages

Sunday, May 12, 2013

Polisi: Bomu Arusha siyo la kienyeji

   Arusha:

Siku saba baada ya tukio la mlipuko wa bomu katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi,Olasiti mkoani Arusha, Jeshi la Polisi limesema kuwa mlipuko huo ulitokana na bomu lililotengenezwa kiwandani.

Taarifa hiyo ni sehemu ya matokeo ya uchunguzi unaofanywa kutokana na tukio hilo lililotokea Jumapili iliyopita, kupoteza maisha ya watu watatu na kujeruhi wengine 67 baadhi wakiwa katika hali mbaya.

Polisi nchini kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola na Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) vipo katika uchunguzi kuhusu tukio hilo lililotokea muda mfupi kabla ya kanisa hilo kuzinduliwa rasmi ambapo mgeni rasmi alikuwa Balozi wa Vatican nchini Askofu Mkuu Francisco Padilla.


Akizungumza na gazeti hili jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Lebaratus Sabas alisema kuwa uchunguzi umebaini kuwa bomu hilo siyo la kutengenezwa kienyeji, bali ni la kiwandani.

“Uchunguzi wa awali unaonyesha, bomu lililotupwa kanisani siyo la kutengeneza kienyeji. Hii ni kwa mujibu wa taarifa tulizozipata kutoka kwa wataalamu ndani ya Jeshi la Polisi,” alisema na kuongeza:

“Taarifa kamili itatolewa Jumatatu (kesho) kwa kuwa kuna baadhi ya watuhumiwa wanaendelea kukamatwa na kuhojiwa na polisi na wengine watafikishwa mahakamani.”

0 maoni:

Post a Comment

Labels