Pages

Friday, April 19, 2013

KIMBEMBE KWA WASIOSAJILI LINI ZAO ZA SIMU


MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kushirikiana na kampuni za simu na vyombo vya usalama imeanza kampeni endelevu yenye lengo la kuwabaini wote wanaotumia namba za simu bila kusajiliwa.

Kampeni hiyo itasaidia kulinda watumiaji wema wa simu na jamii kwa ujumla kwa ajili ya kuimarisha usalama na kuleta maendeleo na ustawi wa wananchi.

Taarifa iliyotolewa kwenye vyombo vya habari iliyotolewa jijini Dar es Salaam juzi ilieleza ni kosa la jinai kwa watumiaji, watoa huduma na wakala wa kampuni za simu kutumia namba za simu ambazo hazijasajiliwa.

Taarifa hiyo iliwataka wote ambao hawajasajili namba zao za simu kufanya usajili mapema ukihusisha taarifa sahihi za mtumiaji, kwani adhabu kwa wasiosajili ni kutozwa faini ya sh 500,000 au kufungwa miezi mitatu jela.

Aidha, taarifa hiyo ilieleza katika vikao vya pamoja vilivyofanyika kati ya Aprili 4 hadi 11 kwa kushirikisha TCRA, Airtel, BOL, MIC (TIGO), Sasatel, TTCL na Vodacom wamekubaliana kwa pamoja kumaliza tatizo la usajili wa namba za simu na kuazimia kufungia namba zote za simu ambazo hazikusajiliwa.

“Kwa mujibu wa kifungu cha 130 cha sheria ya Mawasiliano ya Elektroniki na Posta (EPOCA) ya mwaka 2010, mtu yeyote ambaye anauza au anatoa kwa namna yoyote ile namba ya simu bila kuisajili anatenda kosa la jinai na adhabu yake ni faini ya shilingi 3,000,000 au kifungo cha miezi 12 au vyote,” ilieleza taarifa hiyo.

0 maoni:

Post a Comment

Labels