Pages

Sunday, July 14, 2013

MKE WA NELSON MANDELA | "SINA WASI WASI NA AFYA YA MUME WANGU MANDELA".

MKE wa Nelson Mandela amesema hana wasiwasi na afya ya mumewe kama alivyokuwa wiki moja iliyopita. “Anaendelea kupokea matibabu vizuri,” amesema Graca Machel.

Hata hivyo kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 94 anaelezwa kuwa katika hali mbaya, ikiwa ni wiki ya tano sasa hospitalini. Juzi Rais Jacob Zuma alisema mpambanaji huyo dhidi ya ubaguzi wa rangi wa watawala wachache weupe wa Afrika Kusini “ameendelea kuwa mpiganaji imara hivi sasa kama ilivyokuwa miaka 50 iliyopita.” Alilazwa tangu Juni 8 kutokana na matatizo ya mapafu.
 

Wiki jana, Zuma alikanusha madai kuwa Mandela hivi sasa hajitambui. Watu wengi ambao wamemwona tangu hapo wamekuwa wakisema anajitambua na ana hisia.
BBC imeripoti kuwa Graca amekuwa pembeni mwa kitanda cha Mandela muda wote hospitalini hapo-Medi-Clinic, Pretoria-na amekuwa akijitenga na mgogoro wa kisheria ndani ya familia ya kiongozi huyo ambao umewekwa hadharani katika wiki chache zilizopita.
Graca ni mke wa tatu wa kiongozi huyo mstaafu wa Afrika Kusini, walioana wakati Mandela akitimiza umri wa miaka 80. Rafiki mkubwa Veterani mwingine wa mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi, Ahmed Kathrada, alipata kuruhusiwa kumwona rafiki yake huyo kwa dakika chache.
Kathrada alisema lilikuwa ni tukio la kuhuzunisha kumwona Rais huyo wa zamani, ambaye wakati wakiwa jela pamoja alikuwa na nguvu zake , akiwa katika hali dhaifu kiasi hicho.
Mandela hakuweza kusema lolote, lakini uso wake ulibadilika na kumtambua mgeni wake kupitia machoni, Kathrada alisema alipofika hospitalini hapo Julai mosi akishuhudiwa na Graca.
Hiyo ndiyo taswira ya Mandela ambaye Waafrika Kusini, na watu wengi duniani, wanashindwa kuikubali. Mtu ambaye alivumilia miaka 27 jela na kuongoza nchi yake kuondoka katika mgogoro na kuingia katika maridhiano, hivi sasa yuko mahututi na anafuatiliwa saa zote na madaktari.
Kwa miaka yote tuliyomfahamu, ni mtu ambaye alikuwa akijali sana afya yake, mtu ambaye alifanya mazoezi ndani na nje ya gereza mara zote, na sasa unamwona mtu ambaye ni tofauti kabisa. Si yeye ni ganda lake tu,” alisema Kathrada (83) alipohojiwa Jumatano na AP.
Ulikuwa ni mshituko mkubwa na nilijihisi uchungu, na hatuna la kufanya tumwombee ili aendelee kuwa nasi kwa muda mrefu zaidi,” alisema Kathrada, ambaye aliungana na Mandela katika kipindi kigumu cha mapambano dhidi ya utawala wa wachache.
Wawili hao walikutana mara ya kwanza mwaka 1946, kabla ubaguzi haujaanza. Alhamisi utakuwa ni mwaka wa 50 tangu uvamizi wa mwaka 1963 katika shamba la Liliesleaf jijini Johannesburg, ambao ulikamata wengi wa viongozi wa chama cha African National Congress, wakati huo kikiwa chama cha ukombozi na sasa chama tawala. Kathrada naye alikuwa miongoni mwa waliokamatwa wakati huo Mandela akiwa tayari gerezani.
Ilifuatia kesi ya Rivonia ambayo Mandela alituhumiwa kwa usaliti na kula njama za kupindua serikali, na kutangaza kuwa alikuwa tayari kufa, ikilazimika, kwa imani yake katika usawa wa binadamu.
Yeye, Kathrada na wengine walihukumiwa kifungo cha maisha jela na kupelekwa katika kisiwa cha Robben karibu na Cape Town.
Alikuwa mwanamasumbwi, alikuwa mfanya mazoezi, alikuwa mtu mwenye nguvu,” Kathrada ambaye baada ya ubaguzi wa rangi kwisha alikuwa mbunge, anakumbuka kuhusu Mandela.
“Gerezani pia, tulikuwa tukifanya kazi ya kuponda mawe kwa nyundo na sepetu, tuliona kazi ngumu … lakini yeye alikuwa na nguvu kiasi cha kuizoea mara moja.”
Alimwelezea Graca kama mlinzi mzuri wa geti ambaye anahakikisha wageni, wakiwamo ndugu, marafiki wa zamani na Rais Zuma hawatumii muda mrefu wanapofika hopitalini hapo kumwona mumewe. Mumewe wa kwanza alikuwa Rais wa Msumbiji, Samora Mchel aliyekufa kwa ajali ya ndege mwaka 1986.
Mwanafunzi mwenzake Mwanasheria wa haki za binadamu, George Bizos, ambaye alikuwa mmoja wa wanasheria waliomtetea Mandela na wengine katika kesi ya Rivonia, alisema Graca alimwalika kumwona Mandela mwezi jana. Ziara hiyo hata hivyo, ilifutwa baada ya afya ya rafiki yake huyo kudorora.
“Hakuna kati yetu ambaye hatakufa, lakini nashindwa kuamini kwa uhakika kwamba anaweza kututoka hivi karibuni,” Bizos alisema kwa njia ya simu.
Anakumbuka ziara ya Mandela Johannesburg wiki moja kabla hajalazwa, ambapo wawili hao wakifuatana na Graca, walizungumzia vitu vingi kwa zaidi ya nusu saa, ikiwa ni pamoja na siku zao wakiwa wanafunzi wa sheria Johannesburg.
Kumbukumbu zinaonekana ndani ya nyumba ya Kathrada jijini humo, ambako vifaa vya chakula vya gerezani vimetundikwa ukutani ndani ya fremu. Ni zawadi ya siku ya kuzaliwa kwake aliyopelekewa na Mandela mwaka 1999, ikiwa na maandishi: “Kwa Kathy, kila la heri kwa rafiki yangu wa kweli.”
Picha kubwa ya wawili hao inaning’inia sebuleni. Wote wakitabasamu huku Mandela amemshika Kathrada gotini.
Kabla ya ziara ya wiki jana, kwa mara ya mwisho Kathrada alimwona Mandela Septemba nyumbani kwake kijijini, jimboni Eastern Cape, muda mfupi kabla ya Rais huyo mstaafu hajahamishiwa Pretoria na Johannesburg kwa mara ya kwanza kwa ajili ya kuanza mlolongo wa matibabu.
Kathrada alileta albamu ya picha kutoka Kazakhstan, ambako alikwenda kwa ajili ya tukio la kuenzi fikra za Mandela litakalofanyika Julai 18 siku ya kuzaliwa kwa kiongozi huyo.
Picha hizo zinaonesha watoto ambao walichora michoro inayomwonesha Mandela au bendera ya Afrika Kusini.
Siku yake Maofisa wa Serikali wamekuwa wakiwahimiza Waafrika Kusini kujiandaa kwa sherehe za miaka 95 ya Mandela wiki ijayo. Mandela anajulikana duniani kote kwa mchango wake wa kukomesha ubaguzi wa rangi Afrika Kusini.
Alifungwa jela miaka 27, kabla ya kuachiwa huru mwaka 1990 na kuchaguliwa mwaka 1994 kuwa Rais wa Afrika Kusini. Baada ya kutumikia nafasi hiyo kwa miaka mitano aling’atuka.

0 maoni:

Post a Comment

Labels