Pages

Sunday, March 03, 2013

[MICHEZO]:-WEKUNDU WA MSIMBAZI "SIMBA SC YATOLEWA KLABU BINGWA"

Wawakilishi wengine wa Bara katika michuano hiyo, Simba SC wametolewa baada ya kufungwa mabao 4-0 na Recreativo de Libolo ya Angola kwenye Uwanja wa Manispaa mjini Calulo, Angola.

Matokeo hayo, yanaifanya Simba itolewe kwa jumla ya mabao 5-0, baada ya awali kufungwa bao 1-0 Dar es
Salaam.

Hadi mapumziko, Libolo walikuwa mbele kwa bao 1-0, lakini kipindi cha pili ndipo hali ikawa mbaya zaidi kwa Wekundu wa Msimbazi baada ya kutandikwa mabao hayo matatu na kuwa 4-0.


Simba ilicheza vizuri kipindi cha kwanza, lakini Recreativo walitumia zaidi upande wa kushoto kushambulia, ambako walimzidi beki Amir Maftah na kumgeuza uchochoro.

Na hata bao hilo la kwanza lilitokana na Maftah kuzembea kuokoa mpira hadi mfungaji akaingiza mguu kutokea nyuma yake na kufunga.


Kipindi cha pili, Simba ilifanya mabadiliko, ikiwatoa Amir Maftah na kumuingiza Kiggi Makassy kwenda kucheza beki ya kushoto, wakati Mrisho Ngassa alikwenda kuchukua nafasi ya Chanongo.


Mabadiliko hayo hayakuisaidia Simba SC, kwani Kiggi alikwenda kuwa uchochoro zaidi kuliko Maftah na Libolo wakapitia huko kutengeneza mabao yao, waliyoyapata dakika 15 za mwishoni.


Hata mabeki wa kati nao, waliwaruhusu wachezaji wa Angola kuruka peke yao kwenye mipira mingi ya juu, hivyo kufunga kwa urahisi.

Kikosi cha Simba kilikuwa; Abbel Dhaira, Nassor Massoud ‘Chollo’, Amir Maftah/Kiggi Makassy, Komabil Keita, Juma Nyosso, Shomary Kapombe, Amri Kiemba, Abdallah Seseme, Haroun Chanongo/Mrisho Ngasa, Felix Sunzu na Salim Kinje.

0 maoni:

Post a Comment

Labels